WANANCHI KILIMANJARO WAISHUKURU SERIKALI KUPELEKA MADAKTARI BINGWA WA MACHO.

 

WALIOSUMBULIWA NA MACHO KILIMANJARO WAISHUKURU SERIKALI KUPELEKA MADAKTARI BINGWA WA MACHO.

Na Mwandishi Wetu.

 Same, Kilimanjaro.

Wananchi waliokuwa wakikabiliwa na matatizo ya kuona mkoani Kilimanjaro wameishukuru Serikali kwa kuwaletea madaktari bingwa wa macho kutoka nchini Marekani na kuwafanyia uchunguzi wa magonjwa hayo na ushauri wa kitaalam, tiba kwa upasuaji wa mtoto wa jicho na kuweza kuona upya.

Madaktari hao ambao wamepiga kambi ya wiki mbili katika hospitali ya Wilaya ya Same ambapo watu zaidi ya elfu mbili (2000) wamefanyiwa uchunguzi huku wagonjwa zaidi ya tisini (90) wamefanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti hospitalini hapo mmoja kati ya wagonjwa waliofanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho Bw. Idd Mlaki, Mkazi wa Kileo wilayani Mwanga alieleza kuwa kwa muda wa miezi sita alikuwa haoni tatizo ambalo lilianza ghafla ambapo kwa sasa mara baada ya kupata huduma hiyo hali yake ya kuona imerejea tena.


“Macho yangu yalikufa ghafla nikawa sioni mbele wala nyuma, na ikawa mtu anaponisemesha nilikuwa nakasirika maana sioni na nimehangaika hospitali mbalimbali  bila mafanikio lakini leo nimekuja hapa Same na kukutana na wataalam wakanichuna macho yangu mpaka nikaona tena” alisema Bw. Mlaki.

Mlaki alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuonyesha upendo mkubwa kwa Watanzania na kuendelea kumwomba aendelee kuwasaidia watu wenye uhitaji wa msaada mbalimbali.

Naye Mwanaidi Mdoe mkazi wa Kisiwani wilayani Samwe, alisema kuwa, yeye alikuwa na tatizo la kutokuona jicho moja kwa kipindi cha miaka mitatu ambapo hakupata ufumbuzi lakini kuja kwa wataalam hao imekuwa neema kwake ambapo kwa sasa ameweza kuona tena.

Akizungumzia kuhusu huduma hiyo Mratibu wa macho ambaye ni Kaimu Mganga Mkuu wa wilaya ya Same, Theodora Mwacha alisema kuwa, huduma hiyo ya macho inatolewa na madaktari kutoka Marekani ambapo wanafanya huduma za uchunguzi wa macho na kutoa dawa kwa wagonjwa wenye uhitaji pamoja na miwani.

Theodora alisema kuwa, huduma kubwa wanayoitoa ni huduma ya upasuaji wa mtoto wa jicho ambapo imekuwa faraja kubwa kwa wazee ambao wao ndio wameonekana kukumbwa kwa kiasi kikubwa na tatizo hilo.


“Huduma hii inatolewa bure na wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa wa Kilimanjaro wamefika kuhudumia ambapo zoezi hili linatarajiwa kukamilika Machi 15 mwaka huu na mpaka sasa tumeshawahudumia wagonjwa zaidi ya 2000 huku wagonjwa zaidi ya 90 wamefanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho” alisema Theodora.

 

Mwisho..

Comments

Popular posts from this blog

HATMA YA TAIFA IPO KATIKA USAWA WA KIJINSIA, SIO VIWANDA PEKEE.

MSAKO MKALI KUREJESHA HALI ya USALAMA TANGA, WATUHUMIWA 42 WAKAMATWA

PJT-MMMAM YAWEZESHA UANZISHWAJI WA VITUO 206 VYA MALEZI YA WATOTO WADOGO