DC KASILDA AWAKA UTIRIRISHAJI MAJITAKA YA KIWANDANI KUELEKEA MTONI

DC KASILDA AWAKA UTIRIRISHAJI MAJITAKA YA KIWANDANI KUELEKEA MTONI

Na Musa Mathias,

Same, Kilimanjaro. 

Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Kasilda Mgeni, amepiga marufuku mara moja utiririshaji wa maji machafu yenye kemikali kutoka Kiwanda cha kuchakata mkonge mali kampuni ya Mohammed Enterprises Tanzania Limited (MELT) kilichopo kwenye shamba la mkonge la Hassan Sisal Estate katika kata ya Makanya kwenda kwenye mto unaotumika na wananchi kwa shughuli za kilimo, mifugo na matumizi mengine ya kibinadamu.

Agizo hilo limetolewa kufuatia wasiwasi wa uchafuzi wa mazingira na athari kwa afya za wakazi wa Makanya na maeneo mengine yanayopata maji kupitia mto huo, ambapo awali Mhe. Kasilda alitembelea baadhi ya maeneo na kujionea hali ya maji kwenye mto yaliyokuwa na rangi nyeusi yanayotoa harufu kali, hali iliyomlazimu kufika kiwandani ili kujiridhisha na chanzo cha uchafuzi huo.

"Kuanzia sasa ni marufuku kuelekeza maji machafu yenye kemikali kwenye mto ambao maji yake yanatumika kwenye matumizi mbalimbali ya kibinadamu huko unakoelekea, hasa katika kilimo, mifugo baadhi ya wananchi wanayatumia moja kwa moja," alisema Mhe. Kasilda na kusisitiza kuwa hatua hiyo inalenga kulinda afya za wananchi na mazingira.

Pia, amemwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Same kuhakikisha kuwa wataalam wa mazingira na afya wanakwenda kufanya uchunguzi wa kina kuhusu hali ya mazingira katika kiwanda hicho, kutokana na viashiria vya ukiukwaji wa sheria za kimazingira ili sheria ziweze kuchukuliwa. 

Mhe. Kasilda amesema Serikali anathamini, kulinda na kuweka mazingira wezeshi kwa wawwkezaji lakini ni vema wawekezaji nao wakafuata sheria za uwekezaji wa viwanda wilayani hapa kwa lengo kulinda afya za watanzania na ukuzaji wa uchumi wa wilaya na Taifa kwa ujumla.

Pamoja na mambo mengine Mhe Kasilda ameeleza kutoridhishwa na hali ya usafi kiwandani hapo ambapo amewataka wasimamizi wa kiwanda hicho kuzingatia na kufanya usafi wa maeneo yao ya kazi ili kuepuka magonjwa ya mlipuko yanayoweza kuhatarisha usalama na afya za wafanyakazi.

Kwa mujibu wa sheria ya usimamizi wa mazingira ya mwaka 2004 kifungu cha 129 kinakataza mtu yeyote kuachilia maji taka au taka hatarishi moja kwa moja kwenye mazingira bila kibali au matibabu sahihi.

Hata hivyo, viwanda vinapaswa kuwa na mitambo maalumu ya kutibu majitaka kabla ya kumwaga kwenye mazingira na endapo utatokea ukiukwaji mamlaka ya usimamizi wa mazingira (NEMC) Itachukua hatua.











Baadhi ya picha zikionesha maeneo mbalimbali ndani ya kiwanda cha kuchakata mkonge kilichopo kata ya Makanya wilayani Same. Picha na Musa Mathias. 


Mwisho.

Comments

Popular posts from this blog

HATMA YA TAIFA IPO KATIKA USAWA WA KIJINSIA, SIO VIWANDA PEKEE.

MSAKO MKALI KUREJESHA HALI ya USALAMA TANGA, WATUHUMIWA 42 WAKAMATWA

PJT-MMMAM YAWEZESHA UANZISHWAJI WA VITUO 206 VYA MALEZI YA WATOTO WADOGO