TANZANIA NA SHIRIKA LA IFC KUIMARISHA USHIRIKIANO SEKTA BINAFSI NA UWEKEZAJI
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) zimethibitisha azma ya kuendeleza ushirikiano katika kukuza sekta binafsi, uwekezaji na uchumi endelevu kwa manufaa ya pande zote mbili. Hayo yameelezwa katika mazungumzo kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), na Mkurugenzi wa IFC Kanda ya Afrika Mashariki, Mary Porter Peschka, yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam. Katika mazungumzo hayo, Mhe. Kombo amepongeza mchango mkubwa wa IFC katika kuimarisha sekta ya fedha nchini, hususan kupitia usaidizi kwa benki za NMB, CRDB na NBC. Amesema ushirikiano huo umeongeza upatikanaji wa mikopo na mitaji, na kuwa msaada muhimu kwa wajasiriamali wadogo na wa kati. Aidha, Serikali imetambua mchango wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) katika maendeleo ya miundombinu, ikiwemo huduma za ushauri kwa miradi ya kimkakati kama mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) jijini Dar...