LESENI 73 ZA UTAFITI NA UCHIMBAJI MADINI KUFUTWA.
Na Deborah Lemmubi-Dodoma.
WAZIRI wa Madini Mhe Anthony Mavunde ameagiza kufutwa kwa leseni 73 za utafiti na uchimbaji Madini ambazo Wamiliki wake wameshindwa kurekebisha makosa yao kama vile kutoendeleza maeneo ya leseni zao na badala yake wanahodhi maeneo hayo.
Waziri Mavunde ametoa Maagizo hayo leo Jijini Dodoma November 25,2025 kwa Tume ya Madini wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuelezea mwenendo wa utoaji leseni katila Sekta ya hiyo.
Sambamba na kutoa wito kwa Wamiliki wote wa leseni za Madini kutekeleza matakwa ya Sheria pamoja na masharti ya leseni wanazozimiliki.
"Napenda kuutangazia umma na ninailekeza Tume ya Madini kufuta jumla ya leseni 73 ambazo wamiliki wake wameshindwa kurekebisha makosa na Nitoe wito kwa wamiliki wote wa leseni za madini kutekeleza matakwa ya Sheria pamoja na masharti ya leseni wanazozimiliki kwani Sitawavumilia watu wanaochukua leseni na kukaa nazo bila kuziendeleza. Naielekeza Tume ya Madini kusimamia Sheria kikamilifu na kutoa hati za makosa kwa wakiukaji wote wa Sheria na kufuta leseni zisizoendelezwa bila kumuonea mtu"
Pia Waziri ametumia nafasi hii kuwakaribisha wawekezaji wote nchini wakubwa kwa wadogo wenye nia ya dhati ya kuwekeza katika Sekta ya Madini kuwasilisha maombi ya leseni yaliyokamilika katika maeneo ya wazi, na wao kama Wizara na Tume watawasaidia kuwapatia leseni kwa wakati.
Aidha amesema pamoja na makosa hayo lakini bado kuna mafanikio katika ongezeko la leseni zinazotolewa mwaka hadi mwaka na kuashiria uwepo ongezeko la uwekezaji katika Sekta ya Madini,
kufuatia kuwepo kwa makosa hayo, Tume ya Madini ilitoa Hati za Makosa kwa jumla ya leseni 205, ambazo zinajumuisha leseni za utafiti wa madini 110, na leseni za uchimbaji mkubwa na wa kati 95 ambapo baada ya wamiliki hao wa leseni kupewa Hati za Makosa, baadhi wamewasilisha utetezi wao na kurekebisha makosa, na baadhi wameshindwa kurekebisha makosa yao ikiwemo wamiliki wa Leseni za utafutaji wa madini 44 wameshindwa kurekebisha makosa yao,vilevile wamiliki leseni 29 za uchimbaji wa kati wa madini wameshindwa kurekebisha makosa yao pia.



Comments
Post a Comment