WAZEMBE,WAVIVU SERIKALINI KUKUTANA NA MOTO WA CCM.
Na Deborah Lemmubi-Dodoma.
Katibu wa NEC,Itikadi,Uenezi na Mafunzo Chama cha Mapinduzi Kenani Kihongosi amesema kuwa Chama hicho hakita sita kuchukua hatua kali kwa kiongozi yeyote mzembe ndani ya Serikali iliyoundwa na Chama hicho na kuwataka Wateuliwa wote wajue wana wajibu wa kuwatumikia wananchi na si kinyume chake.
Kihongosi ameyaeleza hayo mapema leo hii Jijini Dodoma November 19,2025 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari akielezea taarifa hiyo ya Chama cha Mapinduzi kwa Umma
Na kusema kuwa wajibu wao kama Chama ni kwenda kusimamia Serikali na sio Serikali kuisimamia Chama kwani ndio kimeunda Serikali hivyo kitakwenda kusimamia kikamilifu.
"Hivyo Chama cha Mapinduzi hakitasita kuchukua hatua kali kwa kiongozi yeyote mzembe ndani ya Serikali ambayo imeundwa na Chama cha Mapinduzi,hivyo tunawataka wote ambao wameteuliwa wajue wana wajibu wa kwenda kuwatumikia wananchi na si vinginevyo".
"Leo nawatangazia rasmi kuwa wajibu wetu kama Chama cha Mapinduzi ni kwenda kusimamia Serikali na sio Serikali kusimamia Chama ambacho kimesimamia kura na kuunda,hivyo Chama kitasimamia Serikali kikamilifu".
Pamoja na hayo pia Kihongosi ametoa Rai kwa Mawaziri,Manaibu Waziri,Viongozi wa ngazi ya Serikali wakiwemo wakuu wa Mikoa,Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri mpaka ngazi chini kwenda kufanya kazi ya kuhakikisha matarajio na maono ya Rais Dkt Samia yanakwenda kukamilika ipasavyo na asiwepo wa kufanya kazi kwa maslahi binafsi.
Yote haya yanakuja katika kuhakikisha uwajibikaji unakuwa ni kipaumbele kwa Watumishi wote wa Serikali kwa manufaa ya Watanzania.


Comments
Post a Comment