MTAMBO WA GESI ASILIA WASAFIRISHWA KWENDA MTWARA KUONGEZA NGUVU YA UZALISHAJI WA UMEME



Na Agnes Njaala, Dar es Salaam

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeendelea kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha upatikanaji wa huduma ya umeme wa uhakika katika mikoa ya Mtwara na Lindi, ili kukidhi ongezeko la mahitaji ya matumizi ya umeme kutokana na ukuaji wa shughuli za kiuchumi na kijamii. 

Hayo yanathibitishwa na hatua zilizochukuliwa na Shirika hilo Kusafirisha mtambo  wa Kuzalisha Umeme kwa Gesi Asilia  megawati 20 unaojulikana kitaalamu kwa jina la TM 2500 kutoka kituo cha Ubungo III jijini Dar es Salaam kwenda Mtwara.

Akizungumza Septemba 11, 2025 wakati wa zoezi la usafirishaji, Mhandisi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme Mtwara II, Godfrey Matiko, alisema mtambo huo una uwezo wa kuzalisha Megawati 20, na utaunganishwa na mtambo mwingine uliopo ambao tayari unazalisha Megawati 20 na hivyo kuongeza jumla ya uzalishaji kufikia Megawati 40 kwenye Kituo cha Uzalishaji Umeme kwa Gesi Asilia kilichopo eneo la Hiyari mkoani humo. 

Amesema, Umeme huo utasambazwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ili kukidhi mahitaji ya matumizi ya umeme yanayoongezeka.

“Usafirishwaji wa mtambo huu unalenga kuongeza nguvu katika kituo cha Mtwara II, hivyo kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na wawekezaji,” alieleza Mhandisi Matiko.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi wa mikoa ya Mtwara na Lindi kujipanga kunufaika na fursa za uwekezaji zitakazochochewa na upatikanaji wa umeme wa kutosha na wa uhakika.

Itakumbukwa kuwa mpaka sasa Mkoa wa Mtwara unauwezo wa kuzalisha umeme jumla ya megawati 50 kwa gesi asilia na uwepo wa mtambo huu mpya wa megawati 20 kutafanya uwezo wa uzalishaji umeme mkoani humo kufikia megawati 70.


Comments

Popular posts from this blog

HATMA YA TAIFA IPO KATIKA USAWA WA KIJINSIA, SIO VIWANDA PEKEE.

MSAKO MKALI KUREJESHA HALI ya USALAMA TANGA, WATUHUMIWA 42 WAKAMATWA

PJT-MMMAM YAWEZESHA UANZISHWAJI WA VITUO 206 VYA MALEZI YA WATOTO WADOGO