TUME YA MADINI YAVUNJA REKODI YA UPIMAJI SAMPULI KWA MWAKA 2024/2025



Maabara ya Tume ya Madini imevuka lengo la upimaji sampuli za madini kwa mwaka wa fedha ulioisha Juni 30, 2024/2025, baada ya kupima jumla ya sampuli 7684 dhidi ya lengo la 6,800.

Hili ni ongezeko linaloashiria ufanisi mkubwa wa maabara katika kutoa huduma kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini.

Akizungumza katika Maonesho ya Nane ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita, Mkemia  kutoka maabara hiyo, David Lyandala amesema maabara inaendelea kutoa huduma za kitaalam za uchunguzi wa madini ili kubaini ubora na kiasi kilichomo. 


Huduma hizo zinajumuisha uchunguzi wa dhahabu, makinikia, kaboni, kimiminika chenye dhahabu, mbale za udongo na miamba kwa kutumia (Fire Assay), pamoja na uchunguzi wa metali kama shaba, chuma, nikeli, manganizi, galena na zinki kwa kutumia mashine za kisasa za X-Ray Fluorescence (XRF).

Aidha, maabara hupima madini ya kinywe (graphite), unyevunyevu wa udongo na miamba, pamoja na upotevu wa uzito kwa kuchoma (Loss in Ignition). 

Lyandala ameongeza kuwa vifaa vya kisasa kama XRF Machine, Atomic Absorption Spectrometer (AAS), CNHS Analyzer na furnaces vimeongeza ufanisi wa huduma, huku wakitoa elimu kwa wadau kuhusu umuhimu wa kupima sampuli kabla ya kufanya maamuzi ya kibiashara.

Kwa upande wake, mchimbaji mdogo kutoka Geita, John Magesa, amesema huduma hizo zimekuwa msaada mkubwa kwa wachimbaji wadogo.

“Zamani tulikuwa tunauza madini bila kujua ubora wake, jambo lililotufanya kupoteza thamani. Sasa tunapata uhakika na tunaweza kufanya biashara yenye faida,” amesema.

Maabara ya Tume ya Madini ipo TIRDO Complex, Kimweri Avenue, Msasani, Dar es Salaam, na inatoa huduma kwa wachimbaji na wafanyabiashara  wa madini kote nchini


Comments

Popular posts from this blog

HATMA YA TAIFA IPO KATIKA USAWA WA KIJINSIA, SIO VIWANDA PEKEE.

MSAKO MKALI KUREJESHA HALI ya USALAMA TANGA, WATUHUMIWA 42 WAKAMATWA

PJT-MMMAM YAWEZESHA UANZISHWAJI WA VITUO 206 VYA MALEZI YA WATOTO WADOGO